Serikali ya Tanzania imepiga marufuku uvutaji wa shisha nchini humo na kulitaka jeshi la polisi kufanya kila juhudi kutokomeza uraibu huo.

Waziri mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa ametoa agizo hilo na kusema uvutaji shisha umekuwa ukichangia katika kudorora kwa maadili miongoni mwa vijana, na kuwapunguzia uwezo wa kiakili na kimwili wa kufanya kazi.

Bw Majaliwa, akiongea katika futari iliyoandaliwa kwenye msikiti wa Khoja Shia Ithnaasheri, Mtaa wa Indira Gandhi jijini Dar es Salaam, amesema watakaokaidi agizo hilo pamoja na wauzaji wa vilevi hivyo, wataadhibiwa vikali.

“Hii (Shisha) ina mchanganyiko mwingi ambao huvutwa na kutoa moshi mwingi, maji yake huwekwa gongo na vilevi mbalimbali hivyo mvutaji hupata ladha mbalimbali ambazo siku akikosa hutafuta mahali popote,’’ alisema Majaliwa.

Awali, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda alikuwa ametangaza kuwa ni marufuku watu kuvuta shisha hadharani iwe ni katika baa, klabu au eneo lolote la starehe.

Alisema Mamlaka ya Chakula na Dawa imebaini kuwa uvutaji wa shisha ni hatari kiafya kwa mtumiaji na watu wanaomzunguka.



Shisha mara kwa mara imekuwa ikidaiwa kutumiwa na watumiaji kwa kuchanganya na dawa za kulevya ikiwemo bangi

Wataalamu wa shisha hata hiyo wanadai kuwa kuna baadhi ya watu wanaotumia shisha vinginevyo na wanafaa kukabiliwa kisheria.

Shisha/sheesha ambayo pia hujulikana kama hookah hutumiwa sana Uarabuni na bara Asia.

Huwa ni tumbaku iliyochanganywa na ladha ya matunda au sukari ya molasi ambayo hujazwa kwenye chombo na moto kuwekwa kati yake. Wakati mwingine maji huwekwa sehemu moja.

Moshi wenye harufu ya ladha iliyotumika hutoka kupitia bomba hilo na kuvutwa kupitia kwenye bomba.
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Karibu tena..wasiliana nasi kwa simu namba 0758059936

Chapisha Maoni

 
Top