Polisi wa Kenya wanamshikilia mtu mmoja mjini Bungoma baada ya kuning’inia kwenye helikopta iliyoubeba mwili wa aliyekuwa mfanyabiashara Jacob Juma.

Mtu huyo, Saleh Wanjala ambaye hakutoa sababu za kufanya hivyo, alishikiliwa na polisi huku akipata matibabu kwenye Hospitali ya Rufaa Bungoma.

Wanjala alionekana akining’inia kwenye helikopta iliyobeba mwili wa mfanyabiashara huyo wakati ikipaa kutoka kwenye Uwanja wa Posta mjini Bungoma baada ya wananchi kutoa heshima za mwisho.

Wanjala aliamua kuidandia helikopta hiyo wakati ikiondoka kupeleka mwili wa Juma nyumbani kwake katika Kijiji cha Mungore.

Akisimulia mkasa huo, Wanjala alisema alikuwa karibu na helikopta hiyo wakati ikianza kupaa na kwamba aliumia baada ya mguu wake kukwama.

“Nilikuwa nimeketi chini ya helikopta na wakati ilipokuwa inaanza kupaa, mguu wangu ulikwama hapo ikabidi nijishikilie vizuri ili nisianguke,” alisema Wanjala.

Rubani wa helikopta hiyo alilazimika kumpeleka hadi uwanja wa ndege wa Bungoma mita 700 kutoka kwenye uwanja huo lakini Wanjala aliamua kuruka na kuumia vibaya miguu na mikono. Muuguzi wa Hospitali ya Bungoma, Leah Atsewa alisema bado wanamfanyia uchunguzi.
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Karibu tena..wasiliana nasi kwa simu namba 0758059936

Chapisha Maoni

 
Top